Msemaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke Bi. Joyce Msumba akiwaeleza waandishi wa Habari juu ya mikakati ya kuimarisha mifumo ya ukusanyaji mapato katika manispaa hiyo ili kuboresha huduma za jamii. Katikati ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari Bi Zamaradi Kawawa na kushoto ni Mhasibu wa Manispaa hiyo Bw. Zakaria Mbedule.(Picha na Frank Mvungi).
Mchumi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke Bw. Edward Simon(kushoto) akitoa ufafanuzi kuhusiana na mikakati ya kuboresha huduma za Jamii ili kuendana na ongezeko la watu katika manispaa hiyo, wakati wa mkutano na waandishi wa habari leo Jijini Dar es salaam. Katikati ni Msemaji wa Manispaa hiyo Bi. Joyce Msumba na kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari Bi. Zamaradi Kawawa.
Halmashauri ya manispaa ya Temeke imefanikiwa kuongeza ukusanyaji wa mapato yake baada ya kuanzisha utaratibu wa kuwa na mameneja wa vyanzo vyote vikubwa na wao kusimamia kwa karibu zaidi.
Katika taarifa yake halmashauri hiyo imesema makusanyo ya mapato ya ndani yameongezeka kutoka shilingi bilioni tatu milioni mia nane tisini na moja na ishirini na tano elfu mia tatu arobaini na sita (3,891,025,346.00) mwaka 2005/2006 hadi shilingi bilioni ishirini na tano, milioni mia moja sabini na tano, hamsini na tatu elfu na tisa (25,175,053,009.00) mwaka 2012/2013.
Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 112.2 ya mapato.
Afisa Uhusiano wa Manispaa ya Temeke Bi. Joyce Peter Msumba akizungumza na waandishi wa habari amesema Halmashauri ya Manispaa ya Temeke inategemea mapato yake kutokana na vyanzo mbalimbali, ikiwemo vyanzo vya ndani, ruzuku kutoka serikali kuu, michango ya wadau mbalimbali wa maendelo na wahisani , pamoja na nguvu za wananchi, ikiwa ni kwa mujibu wa sheria ya fedha ya serikali za mitaa (Local Government Finance Act Na. 8 ya mwaka 1982).
Aidha Bi Msumba amesema pamoja na mafanikio yaliyopatikana lakini bado ziko changamoto wanazokabiliana nazo ikiwemo Ongezeko la idadi ya watu; hasa wahamiaji kutoka katikati ya jiji na kutoka mikoa mingine kuhamia Manispaa ya Temeke na pia Ongezeko la uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na utupaji ovyo takataka.
Ameomgeza kuwa changamoto nyingine ni kuchelewa kwa ruzuku kutoka Serikali kuu na wahisani na Ujenzi holela wa makazi.
Manispaa ya Temeke ni moja kati ya Halmashauri zinazounda Jiji la Dar-es-Salaam, nyingine ni Ilala na Kinondoni, ina eneo la kilometa za mraba 656 na ukanda wa pwani wa kilometa 70.