Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia kwa Afrika Makhtar Diop.
Benki ya Dunia imetoa changamoto kwa nchi za Afrika kuhimiza maendeleo endelevu ya ardhi ili kupunguza umaskini na kujiletea maendeleo.
Ripoti ya Benki hiyo imeeleza kuwa ingawa nchi za Afrika zina karibu nusu ya eneo la ardhi nzuri ambayo haijaendelezwa kwa kilimo, bara hilo limeshindwa kuiendeleza ardhi hiyo inayokadiriwa kuwa hekta milioni 202 kujikwamua katika umaskini, kuleta maendeleo ya uchumi, kuongeza nafasi za kazi na kuleta mafanikio kwa jumla.
Ripoti hiyo inayoitwa “Kutumia ardhi ya Afrika kwa mafanikio ya pamoja,” inaeleza kuwa nchi za Afrika na jamii zake zinaweza kabisa kuondoa tatizo la uporaji wa ardhi, kuzalisha mazao ya chakula na kubadilisha taratibu za usimamizi na umiliki wa ardhi katika mwongo ujao.
Ripoti hiyo imeeleza, Afrika ina kiwango kikukbwa cha umaskini ambapo asilimia 47.5 ya watu wake wana kipato chini ya dola 1 za Marekani ($1.25)kwa siku.
Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia kwa Afrika Makhtar Diop amesema licha ya kuwa na ardhi kubwa na utajiri wa madini, Afrika bado ni maskini.
Ameongeza kuwa kuboresha usimamiaji wa ardhi ni muhimu kwa maendeleo ya haraka na kutoa nafasi zaidi kwa waafrika, wakiwemo wanawake ambao ni asilimia 70 ya wakulima wa Afrika, ambao wanakwazwa kumiliki ardhi na sheria za kimila na kuwa hali hii haikubaliki na lazima ibadilike ili waafrika waweze kunufaika na ardhi yao.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa zaidi ya asilimia 90 ya ardhi haijarasimishwa, hivyo kuwa na hatari kubwa ya uporaji na kuchukuliwa kwa malipo ya chini ya fidia.
Hata hivyo kumekuwa na matumaini ya maboresho chini ya mipango inayoendelezwa katika nchi za Ghana, Malawi, Msumbiji,, Tanzania, na Uganda, ambapo mpango wa kutumia ardhi kwa mafanikio ya pamoja unaweza kuleta mapinduzi ya uzalishaji wa kilimo na uporaji wa ardhi na kuondoa umaskini wa kutupa barani Afrika.
Ripoti hiyo inapendekeza kuwa Afrika inaweza kufanikiwa kuendeleza ardhi yake katika kipindi cha muongo ujao kwa na mabadiliko na uwekezaji, kurasimisha ardhi na maeneo muhimu yanayomilikiwa na watu binafsi.
Pia kusimamia taratibu za umiliki za maeneo yaliyovamiwa na kujengwa bila mpangilio mijini ambapo wanaishi zaidi ya watu asilimila 60 barani Afrika na kukabiliana na udhaifu wa utawala na rushwa katika mfumo wa usimamizi wa ardhi katika nchi za Afrika ambao, kwa kawaida unapendelea wakubwa na kuathiri maslahi ya wananchi walio maskini.
Akifafanua zaidi Makhtar Diop amesema Serikali za Afrika zinatakiwa kuwa na dhamira ya kisiasa kuhimiza mabadiliko haya ya ardhi kuvutia raslimali na uwezekezaji wa jamii ya kimataifa. .
Ripoti hiyo inasema kuwa mpango huo utagharimu nchi za Afrika na washirika wa maendeleo , ikiwemo sekta bianfsi kiasi cha dola za Marekani bilioni 4.5 katika kipindi cha miaka 10 kuleta mabadiliko ya sera na uwekezaji.